Thursday, July 31, 2008

mazishi ya wangwe yaahirishwa kwa ghasia








Mazishi ya Mh. Chacha Wangwe, aliyekuwa Mbunge wa Tarime aliyefariki dunia kwa ajali ya gari majuzi huko Dodoma, yameshindwa kufanyika leo kijijini kwake Kamokorere baada ya kufumuka kwa vurugu kubwa ambapo wabunge na viongozi wa serikali na vyama vya siasa walohudhurian ilibidi watoke bomba kusalimisha maisha yao.
Vurugu hiyo ilianza dakika chache baada ya kuwasili kilioni hapo kwa Mwenyekiti wa Taifa wa CHADEMA, Mh. Freeman Mbowe, katika kijiji cha Kemokorere kiasi cha kilomita 20 hivi toka mjini Tarime.
Hali ilipokuwa mbaya, ilibidi Mh. Mbowe na viongozi wote waliohudhuria mazishini waondolewe kilioni chini ya ulinzi mkali wa FFU ukiongozwa na Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Mara Afande Leberatus Barlow ambao walifanya kazi ya ziada kuepusha balaa.
Viongozi wengine waliohudhuria walikuwa ni pamoja na wenyeviti wa vyama vya upinzani Profesa Ibrahim Lipumba (CUF), Augustino Lyatonga Mrema (TLP), John Cheyo (UDP) James Mbatia (NCCR-Mageuzi) na Mbunge wa Karatu Mh. Wilbroad Slaa pamoja na kiongozi wa upinzani bungeni, Mh. Hamad Rashid.
Wote hao walisindikizwa chini ya ulinzi mkali wa FFU kuondoka mahali hapo na kuelekea Musoma. Waziri wa Kilimo na Umwagiliaji, Mh. Steven Wassira, na Manaibu Mawaziri ambao ni wabunge wa Kanda ya Ziwa, Dr. James Wanyacha na Gaudensia Kabaka nao ilibidi waondoke.
Ujumbe toka Kenya ulioongozwa na Dr Wilfred Machage ambaye ni mbunge wa jimbo la Kurya na pia Naibu Waziri katika serikali ya mseto ya Kenya pamoja na wakuu wa wilaya wawili nao walikuwepo na ilibidi waondoke kwa kuruka ukuta.
Tofauti na walivyoingia, itifaki haikuweza kufuata kama walipowasili wabunge 20 wakiongozwa na mbunge wa Bumburi Mh. William Lukindo vurugu hilo lilipoanza na ilibidi kila mmoja aondoke chini ya ulinzi mkali.
Maelfu ya waombolezaji, wengi wao wakiwa vijana waliobeba mabango yenye ujumbe mbalimbali unaohoji kifo cha Mh. Wangwe, walitawala hapo kilioni. Juhudi za Mkuu wa mkoa wa Mara Mh. Issa Machibya kuwatuliza hazikuzaa matunda.
Hata juhudi za kututuliza ghasia hizo za Wah. Zitto Kabwe na mmoja wa wanafamilia waandamizi kama vile Profesa Samwel Wangwe na Mkuu wa zamani wa Halmashauri ya Tarime Mh. Peter Wangwe pia hazikuambulia kitu.
Prof Wangwe aliwaambia waombolezaji hao wenye hasira kwamba familia ya Wangwe imeamua kumtafuta mtaalamu huru kuifanyia upya uchunguzi maiti ya hayati Chacha Wangwe ili kubaini alifariki kwa njia ipi.
Wengi ya waombolezaji wanatuhumu kwamba Mh. Wangwe hakufa kwa ajali ya gari. Mtu moja aliyekuwa na marehemu wakati wa ajali, Bw. Mallya, anahojiwa na polisi na uchunguzi wa kina unaendelea.

Source: www.michuzi-blog.com



1 comment:

Anonymous said...

hi, new to the site, thanks.