Friday, February 19, 2010

Waumini wa Kakobe wacharuka

WAUMINI wa Kanisa la Full Gospel Bible Fellowship (FGBF) jana waliwazuia watumishi wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kuweka nguzo zenye msongo mkubwa wa kilovolti 132 karibu na kanisa hilo tukio ambalo nusura lizue vurugu, lakini Polisi wakawahi eneo hilo na kutuliza hali hiyo.
Tukio hilo lilitokea saa tano asubuhi baada ya wafanyakazi wanaosadikiwa kuwa ni watumishi wa Tanesco kwenda eneo hilo na gari lenye namba za usajili T346 ARR kwa lengo la kusimika nguzo hizo, lakini hata hivyo walikutana na upinzani mkubwa kutoka kwa waumini hao.
Mashuhuda wa tukio hilo walisema walivyofika walisimamisha gari eneo hilo tayari kuanza kazi, lakini hata hivyo waumini wa kanisa hilo ambao wanapeana zamu za kulinda kanisa hilo, waliwazuia wasifanye lolote. Jana kulikuwa na waumini takribani 200 ambao walikuwa zamu ya asubuhi.
Kiongozi wa kanisa hilo, Askofu Zacharia Kakobe alikiri waumini wake kuwazuia wafanyakazi wa Tanesco kusimika nguzo hizo kwa maelezo kuwa bado mazungumzo kati yake na wadau wengine ikiwemo serikali yanaendelea hivyo haoni haja kwa nini zitumike nguvu kuweka nguzo hizo. “Nimeambiwa na wizara nipeleke maoni yangu na mwisho ilikuwa jana, iweje hawa leo waje kuweka nguzo wakati hakuna tangazo lolote la serikali? Alihoji Kakobe na kueleza kuwa yawezekana kuna watu ambao wanania ya kuchochea vurugu kwa lengo la kuipaka matope serikali. Askofu huyo alisema baada ya vuta nikuvute baina ya watumishi hao na Tanesco, polisi walifika wakiwa kwenye magari tayari kwa ajili ya kutuliza ghasia, lakini gari hilo la Tanesco liliondolewa na watumishi hao. Polisi walifika eneo hilo wakiwa kwenye magari matatu tayari kutuliza ghasia hizo kutokana na waumini wa kanisa hilo kuapa kwamba nguzo hizo haziwezi kuwekwa hapo kwa sababu ya zina madhara kwa afya zao na kwa vyombo vya mawasiliano vya kanisa hilo ikiwemo kituo cha televisheni ambacho wako mbioni kukianzisha. Polisi walipofika eneo hilo na mafundi hao kuondoa gari kwa kasi na kuondoka, kiongozi wao ambaye jina lake halikupatikana alisema angefuatilia kuona sababu ya mafundi hao wa Tanesco kuondoka eneo hilo.
Meneja Mawasiliano wa Tanesco Badra Masoud, alikiri kuwepo kwa tukio hilo, lakini akasema waliozuiwa kufanya kazi ni kampuni iliyoajiriwa na Tanesco kusimika nguzo hizo ijuliakanyo kama Takawoka. “Wale waliozuiwa sio Tanesco ni kampuni tuliyoiajiri kusaidiana na sisi kuweka nguzo zile, pale walienda kwa ajili ya kusafisha na kufanya maandalizi ya kuweka nguzo,” alisema Masoud na kukanusha kuwa watu hao walienda hapo kuweka nguvu. “Lile eneo mimi silizungumziii kabisa kwa sasa, lakini kazi yetu ya kuweka nguzo inaendelea huku Kijitonyama kwani hakuna malalamiko kama pale, lakini pia nikuhakikishie kuwa uwekaji wa nguzo uko maeneo mengine na sio pale,” alisema Badra.
Source: habari leo

Waumini wa Kakobe watimua wahandisi wa Tanesco

Mgogoro kati ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) na waumini wa Kanisa la Full Gospel Fellowship kuhusu kupitisha njia ya umeme wa msongo wa Kilovoti 132 mbele ya kanisa hilo, umechukua sura mpya, baada ya waumini hao kuwatimua wahandisi wa shirika hilo waliokwenda kufanya tafiti.
Tukio hilo lilitokea jana saa 6:30 mchana, baada ya wahandisi hao wakifuatana na polisi kufika eneo la kanisa hilo lililopo Mwenge kwa ajili ya kuanza utafiti kuhusu athari zitakazotokea umeme huo utakapopitishwa.
Mratibu wa Mgogoro huo kwa upande wa kanisa hilo, Emmanuel John, alisema watu hao ambao walijitambulisha kuwa wanatoka Kampuni ya Dico na Tanesco walifika eneo hilo na kueleza kuwa walikwenda kwa ajili ya kufanya utafiti wa athari zitakazopatikana kwa binadamu, jengo na vifaa vya kanisa hilo.
Alisema, kabla ya tukio hilo, juzi walipokea fax kutoka Wizara ya Nishati na Madini ikiwataarifu kuwa itatuma jopo la wahandisi kwenda kufanya utafiti, lakini haikueleza siku na saa ambayo watu hao watafika.
Alisema mtafaruku uliibuka baada ya waumini kuwaarifu wahandisi hao kwamba hawawezi kuwaruhusu kufanya kazi hiyo bila kuwepo kwa Askofu Kakobe, kwani muda huo hakuwepo.
"Waumini walipinga kufanya kazi hiyo ikiwa Askofu Mkuu hayupo, lakini wenzetu walikuwa wabishi wakataka kuenndelea na kazi zao kitu ambacho kilileta mvutano mkali," alisema.
Baada ya mvutano wa muda mrefu, waliamua kumpigia simu Askofu Kakobe ili wajadiliane na watu hao, ambapo baada ya majadiliano hayo iliamuriwa wahandisi hao warudi walipotoka na kazi hiyo ifanyike leo wakati askofu huyo akiwepo.
Mgogoro huo unaodumu kwa miezi miwili sasa umesababisha waumini wa kanisa hilo kuanzisha ulinzi nje ya kanisa kupinga hatua yoyote ya Tanesco kutekeleza mradi huo.
Source: Nipashe