Wednesday, March 16, 2011

Mwingira amlaani mchungaji Loliondo

Mtume na Nabii Josephat Mwingira wa Kanisa la Efatha amemuombea mabaya Mchungaji Ambikile Mwasapile anayetoa tiba ya magonjwa sugu katika eneo la Samunge, Loliondo kwamba anapaswa kulaaniwa hadi kufa kutokana na kutoa huduma hiyo.

Mwingira alisema hayo katika mahubiri ya ibada ya Jumapili aliyoyatoa katika Makao Makuu ya Kanisa hilo lililoko Mwenge jijini Dar es Salaam. “Imeandikwa katika Biblia kwamba,ukipewa bure nawe toa bure. Iweje yeye anauza dawa hiyo, ikiwa Mungu amesema aponye watu. Hakuna sababu ya kuwatoza fedha yoyote wagonjwa.

“Hizi ni roho za kishetani zinazotaka kuwaangusha walio wengi ambao hawamjui Yesu Kristo kwani haiwezekani mtu atumiwe na Mungu halafu hata siku moja asimtaje Yesu. Asitumie Biblia hata kuwahubiria watu wamtumaini muumba wao,”alisema Mwingira.

Mwingira alisema huduma hiyo ni uongo na kwamba haina tofauti na Deci iliyokuja kiujanja ujanja na kuteka watu wengi baadaye walijutia maamuzi yao. “Kama mpakwa mafuta wa Bwana niliyeitwa kwa kusudi lake.

Nailaani Loliondo ife pamoja na Mchungaji wake na itoweke kama Deci ilivyotoweka,” alisema Mwingira. Mwingira alisema Mchungaji Mwasapile ni mwongo, anataka kuwadanganya watu na kuwapoteza kiimani.

Alisema kama alivyoilaani Deci na ikafa, anailaani huduma ya Loliondo ili ife kwa kuwa mchungaji huyo ni roho ipotezayo, inayotaka kuwateka watu walioko gizani na kuwaangamiza. Alisema baadhi ya viongozi tayari wamepigwa ngwara na roho hiyo na kunywa dawa, bila wao kujijua.

“Sitakubali kuendelea kuona roho hiyo ikipoteza watu. Nailaani itoweke Loliondo na iangamie kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti,”alisisitiza. Mwingira alisema haiwezekani kwa mtu aliyeitwa na Mungu kuwahudumia watu wake, baadhi ya watu hao wafe kwenye huduma yake.

“Ni wagonjwa wangapi wamepelekwa kule na wengine wamefariki nyumbani kwake kabisa na wengine njiani, je mlishawahi kujiuliza? alihoji Mwingira. Mwingira alitoa kauli hiyo siku chache baada Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo kulieleza gazeti hili:"Miujiza haiji kwa urahisi hivyo na watu kuponya kiasi hicho, huenda wanaweza kuponywa kwa ‘Illusion’ na baade ikaleta madhara."

Alisema cha msingi watu wanapaswa kuwa makini na serikali pia kwa sababu, wingi wa watu kuponywa huenda baadaye ukaleta vifo vingi zaidi kutokana na dawa yenyewe.


Pengo alisema: “Ninachoamini miujiza haiji kwa urahisi na watu wakaponywa kiasi hicho kwa mara moja, huenda ikawa ni kuponya kwa ‘illusion’ na baadae watu wakapata madhara makubwa.

“Ila sina jibu la kutoa kuhusu uponyaji huo, nabaki tu kushangaa nayayotendeka kwa Mchungaji huyo hadi kufikia watu kuamini kiasi hicho,”alisema. Pengo alisema huenda akawa ameamua kutumia njia hiyo akawavuta hata wa waumini waingie kwenye imani yake na kuacha dini zao.

Source:mwananchi.co.tz

Lowassa apata kikombe Loliondo

WAZIRI Mkuu wa zamani, Edward Lowassa juzi alipata tiba ya magonjwa sugu inayotolewa na Mchungaji Mstaafu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Ambilikile Mwasapile katika Kijiji cha Samunge, Tarafa ya Sale, Loliondo, mkoani Arusha.Lowassa alifika katika eneo hilo mchana akiwa na viongozi kadhaa wa Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro na Serikali kisha kupata kikombe kimoja chenye dawa kinachotolewa na mchungaji huyo kwa ajili ya tiba.

Tofauti na viongozi wengine, Lowassa ambaye ni Mbunge wa Monduli (CCM), Jimbo linalopakana na Kijiji cha Samunge, alikwenda huko akiwa na viongozi mbalimbali wakiwamo viongozi wa dini na baadhi ya wapigakura wake.

Akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu jana, Lowassa alithibitisha kwenda Loliondo na kuwataja viongozi wa dini alioambatana nao katika msafara wake kuwa ni Askofu Msaidizi wa KKKT, Dayosisi ya Kaskazini, Dk Frederick Shoo na Mkuu wa Jimbo la Masai Kaskazini, Dayosisi ya Kaskazini Kati (Arusha), Mchungaji John Nangole.

Katika ramani ya utendaji kazi ya KKKT, Jimbo la Masai Kaskazini ndipo kilipo Kijiji cha Samunge ambako ni makazi ya Mchungaji Mwasapile.“Ni kweli, nimekwenda pale na wapigakura wangu pamoja na viongozi wa dini, Msaidizi wa Askofu wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini, Dk Shoo na Mkuu wa Jimbo la Masai Kaskazini, Mchungaji Nangole,” alisema Lowassa na kuuliza: “Kwani hiyo nayo ni habari jamani?”

Baada ya Lowassa kufika katika kijiji hicho akiwa na ujumbe wake, aliongoza moja kwa moja hadi kwa Mchungaji Mwasapile na kuzungumza naye kisha akapata kikombe cha tiba na kuondoka.

Kabla ya Lowassa kwenda kupata tiba, amekuwa akitoa msaada wa nauli kwa wagonjwa mbalimbali wa jimbo lake kwenda kwa mchungaji huyo ambaye dawa yake inadaiwa kutibu magonjwa ya saratani, kisukari, pumu, shinikizo la damu na Ukimwi.Lowassa ni miongoni mwa wanasiasa maarufu nchini ambao wameshafika kwa mchungaji huyo kupata tiba hiyo wakiwamo mawaziri, naibu mawaziri, wabunge, wakuu wa mikoa na wilaya.


Katika jitihada za kudhibiti usalama na kuhakikisha kwamba wananchi wanapata huduma kwa mchungaji huyo bila matatizo, Serikali imeimarisha ulinzi kwa kuweka askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), katika kijiji hicho na kusimamia magari. Pia imepeleka wauguzi kusaidia wagonjwa mahututi kabla ya kumfikia mchungaji na imetoa pia jenereta kwa ajili ya kufua umemeKaimu Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Raymond Mushi alisema jana kuwa, sasa walau hali ni nzuri kwani msongamano umepungua.


"Ni kweli sasa hali inaridhisha na jana watu wamekwenda kupata tiba na kurejea makwao mapema hili ndilo serikali inalolitaka. Tunaomba watu wanaopeleka wagonjwa wawe wanauliza kwanza hali ya msongamano," alisema Mushi.Mushi alisema inawezekana watu wanaokwenda katika kijiji hicho kusubiriana katika Mji wa Mto wa Mbu ambako kuna huduma nyingi muhimu kuliko wote kwenda huko kwa wakati mmoja.

Alitoa wito kwa watu wenye wagonjwa mahututi kuacha kuwapeleka moja kwa moja kwa mchungaji huyo kabla ya kupata ushauri wa kitaalamu kuhusu afya zao.Katika hatua nyingine, wagonjwa kadhaa waliolazwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili wameanza kutoroka wodini na kwenda Loliondo kupata matibabu ya magonjwa sugu yanayotolewa na Mchungaji Mstaafu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Ambilikile Mwaisapile, Mwananchi imeelezwa.

Habari zilizopatikana hospitalini hapo jana zimeeleza kuwa wagonjwa hao walianza kuondoka Muhimbili juma lililopita baada ya Serikali kubariki matibabu hayo. Ofisa mmoja mwandamizi wa hospitali hiyo ambaye aliomba jina lake lisiandikwe gazetini, amesema kuwa wakati baadhi ya wagonjwa hao wakiwa wanatoroka wodini, wengine wamekuwa jasiri kwa kuwaaga madaktari wao.

“Wagonjwa wameanza kuondoka na wengine bila hata ya kuaga, hivyo hatujui hatima yao kama watafika salama huko Loliondo,” alisema.Ofisa huyo alisema juma lililopita, mgonjwa mmoja aliyekuwa amelazwa chumba namba 15 katika Wodi ya Kibasila, aliondoka baada ya kusikia taarifa kuhusu huduma hiyo.

“Kuna mgonjwa mmoja aliyekuwa amelazwa Kibasila Wodi namba 15 aliondoka aliposikia kuwa Babu ameanza tena kutoa matibabu hayo ambayo awali yalisitishwa,” alisema.Hata hivyo, Ofisa Habari wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Aminiel Aligaisha alisema hana taarifa za kutoroka wodini kwa wagonjwa hao na kwenda kufuata tiba huko Loliondo... “Sina taarifa zozote za kuondoka kwa wagonjwa hapa hospitalini.”

Matibabu Loliondo yapandisha nauli Ubungo
NAULI za kwenda Arusha kutoka Ubungo, Dar es Salaam zimepanda kwa kasi katika siku za hivi karibuni kutokana na wingi wa wasafiri wanaoelekea Loliondo kupata tiba hiyo ya magonjwa sugu.Habari zilizolifikia gazeti hili jana kutoka kituoni hapo zimeeleza kuwa, nauli hizo zimepanda kutoka Sh18,000 hadi Sh30,000 tangu juma lililopita.

Mmoja wa mawakala wa mabasi ya abiria katika kituo hicho ambaye hakutaka kutajwa gazetini alisema ongezeko hilo la nauli limetokana na baadhi ya mawakala kukodi mabasi na kuwasafirisha abiria.“Nikupe siri moja tu ambayo inatufanya tupandishe nauli. Lengo letu ni kupata faida, ujue sisi tunakodi basi zima kisha tunakatisha tiketi kwa bei yetu ili na sisi tupate faida,” alisema.

Mmoja wa abiria aliyekuwa akisafiri kuelekea Arusha, Charles Manyama alisema mabasi yaendayo huko yamegawanyika katika madaraja matatu yale ya bei ya juu, bei ya kati na bei ya chini lakini kwa sasa bei imekuwa ni moja kwa mabasi yote.

Kwa mujibu wa abiria huyo, zamani nauli za Arusha zilikuwa Sh25,000 kwa basi la daraja la juu, Sh18,000 kwa mabasi ya daraja la kati na Sh15,000 kwa daraja la chini, lakini sasa mabasi yote yanatoza kati ya Sh25,000 hadi Sh30,000.“Mawakala hawa wanadhani kila mtu anayepanda magari haya anakwenda Loliondo lakini siyo kweli, wengine tuna safari nyingine kabisa," alisema Manyama na kuongeza:

"Unakuta bei zinashangaza na kupanda sana. Hata hivyo, inashangaza kuona wanadamu tunakosa utu. Watu wanakwenda kupata matibabu wanapandishiwa nauli, walipaswa kuwaonea huruma wagonjwa hawa,” alisema Manyama.Jitihada za kumtafuta Meneja wa kituo cha mabasi Ubungo ziligonga mwamba baada ya taarifa kutoka ofisi kwake kueleza kuwa alikuwa nje kikazi.

Polisi Arusha wadhibiti usafiri wa Loliondo
Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha limeitaka Halmashauri ya Jiji la Arusha kuweka vituo vinavyotambulika kwa ajili ya wagonjwa wanaokwenda kupata matibabu kwa Mchungaji Mwasapile ili kuepuka utapeli.

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Akili Mpwapwa alisema jana kuwa kutokana na idadi kubwa ya watu kutaka kwenda Loliondo, kumezuka vituo vingi ambavyo vinaweza kuwa chanzo cha utapeli kwa watu wanaotoka mikoani."Nafahamu hili ni jambo ambalo manispaa wanahusika nalo, wahakikishe kuwa hakuna vituo visivyo rasmi ili wananchi wasije kudanganywa na watu wabaya," alisema.

Katika kituo kilichoibuka ghafla baada tiba ya magonjwa sugu kuanza kutolewa cha Chini ya Mti, kulizuka vurugu za madereva na madalali waliokuwa wakibishania kiwango cha nauli, hatua iliyosababisha polisi wenye silaha kupelekwa katika eneo hilo.

Hatua ya polisi kuonekana katika kituo hicho, ilisababisha wasiwasi kwa wananchi kuwa huenda Serikali imesimamisha utaratibu wa wananchi kwenda Loliondo, jambo ambalo kaimu kamanda huyo alilikanusha.

"Tunachokifanya ni kuweka utaratibu mzuri, polisi wanasimamia sheria. Magari mengine yanazidisha idadi ya watu na kutoza pesa nyingi zaidi. Sumatra wakisema nauli sahihi ni kiwango fulani na madereva wakizidisha basi tunawakamata," alisema.

Wananchi waliozungumza na gazeti hili bila kutaja majina yao walisema kuwa wanashangazwa na bei ya nauli kuwa juu hata baada ya Serikali na KKKT, Dayosisi ya Kaskazini Kati kuboresha mazingira ya kuwahi kupata tiba na kuondoka kijijini Samunge.

"Mwanzoni walikuwa wanasema magari yanakaa sana huko, kwa hiyo wanafidia hizo siku za kungoja wagonjwa lakini sasa hivi ukienda leo unarudi kesho na nauli bado iko juu," alisema mmoja wa wananchi hao.Nauli ya kutoka Mjini Arusha hadi Samunge, Loliondo ni Sh100,000 kwenda na kurudi kwa magari aina ya Land Cruser ,huku nauli ya mabasi ikiwa pungufu zaidi.

Source: mwananchi.co.tz

Saturday, March 12, 2011

Yanayojiri sayuni

Anonymous DORAH said...

NILIKUWA muumini wa kanisa la EAGT MNAZI MMOJA..CHINI YA MCHUNGAJI andrew.naomba nifahamishwe kanisa hilo limehamia wapi..nikija TANZANIA NAHANGAIKA KUTAFUTA SEHEMU YA KUABUDU..NAOMBA TAARIFA.

March 10, 2011 12:48 AM

Delete
Blogger Mtade said...

Mtumishi Dora, Kanisa la Pastor Andrew kwa sasa lipo mnazi mmoja kati ya jengo la ushirika lumumba na ilipokuwa sukita zamani.Kuna jengo jeupe la ghorofa saba.karibu kabisa na mabasi ya hekima au sumry yanayotokea mbeya.Ukifika hapo pandisha ghorofa ya tatu utakuwa umefika.Kanisa linaitwa faith word church.Kwa maelezo zaidi ukifika piga namba hii utafika 0713-427857

Barikiwa

March 12, 2011 4:07 PM

Loliondo kwa babu

Msafara wa magari kuelekea Loliondo kwa Mchungaji Ambilikile Mwasapile.

WAKATI Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Haji Mponda akieleza kuwa ameagiza Serikali ya Mkoa wa Arusha kuzuia tiba ya magonjwa sugu inayotolewa na Mchungaji Ambilikile Mwasapile, Kaimu Mkuu wa Mkoa huo, Raymond Mushi amesema ni vigumu kusitisha huduma hiyo.

Mushi alisema pamoja na kutopata barua yoyote inayomwagiza asimamishe huduma za mchungaji huyo, ni vigumu katika mazingira yaliyopo katika Kijiji cha Samunge, Loliondo kufanya hivyo ikizingatiwa kwamba hivi sasa kuna maelfu ya watu hasa wagonjwa walioko hapo na wengine wakiendelea kumiminika.

“Hata mimi nimemsikia Waziri Dk Mponda, lakini siwezi kuanza kufanya kazi bila kupokea barua na maelekezo. Lakini hili jambo ni gumu kidogo kwani watu bado wanakwenda na tukipata barua tutajua jinsi ya kukabiliana na hali hii,” alisema Mushi.

Kaimu Mkuu huyo wa Mkoa alisema kama akipokea barua na maelekezo watakaa na watendaji wengine kuona ni jinsi gani wataweza kukabiliana na hali ya Loliondo. “Pale yule mchungaji anasema anatoa huduma ya tiba na lile jambo ni la kiimani ndiyo sababu anasema wenye imani watapona sasa sidhani kama wataalamu wakipeleka dawa ile maabara wataona kitu,” alisema Mushi.

Mbali ya Kaimu Mkuu wa Mkoa kuonyesha wasiwasi wake juu ya utekelezaji wa agizo hilo la Waziri, Mbunge wa Ngorongoro (CCM), Saning’o ole Telele amepinga hatua hiyo ya serikali kutaka kuzuia kwa muda tiba hiyo akisema badala yake, inapaswa kusaidia watu kupata tiba.“Sikubaliani na Waziri wa Afya kuzuia tiba eti sijui mchungaji ajisajili kwanza.Tunachoomba ni serikali kusaidia watu wafike Ngorongoro, Samunge na kupata tiba katika mazingira bora,” alisema Telele.

Telele alisema watu wengi wamepona kwa kunywa dawa hiyo, hivyo Serikali inapaswa kuomba msaada wa mashirika mbalimbali kama Msalaba Mwekundu yafike kuweka mahema na kutoa huduma ya kwanza.Jana, Dk Mponda alimtaka Mkuu wa Mkoa wa Arusha, kuzuia mara moja matibabu ya magonjwa sugu yanayoendeshwa na Mchungaji Mwasapile hadi serikali itakapojiridhisha ubora na usalama wake kwa watumiaji.

Akizungumzia tamko hilo la Waziri, Msaidizi wa Mchungaji Mwasapile, Paulo Dudui alisema amepotoshwa kwa vitu vingi: "Kwanza siyo kweli kuwa wagonjwa wote wanatumia kikombe kimoja na pia si kweli kwamba wanatumia maji ya mto."

"Kila mgonjwa anatumia kikombe chake na tuna vikombe zaidi ya 100 ambavyo baada ya kutumika vinaoshwa na wagonjwa wanaona na pale kuna maji ya bomba yanayotoka katika chanzo cha maji cha Samunge.”Lakini Dudui alisema kama wakipokea maelekezo ya serikali kuhusu tiba watakaa na kujadiliana kwani wanaamini huduma ambayo wanatoa ina manufaa makubwa kwa watu na siyo uganga.

“Mchungaji mwenyewe atasema nini cha kufanya ila Waziri kapotoshwa. Hapa serikali ilitakiwa kusaidia huduma kutolewa na siyo kuzuia,” alisema Dudui.Katika hatua nyingine Dudui alisema kwamba mtoto mmoja alifariki dunia jana katika eneo hilo kutokana na kuchelewa kupata tiba.


Source: http://www.globalpublishers.info

Tuesday, March 8, 2011

Ya Mchungaji wa Loliondo

WAKATI idadi ya watu ikizidi kumiminika katika Kijiji cha Samunge, Tarafa Sale, Loliondo kupata kile kinachoaminika kuwa ni tiba dhidi ya magonjwa sugu, mtoa huduma hiyo, Mchungaji Mstaafu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri (KKKT), Ambilikile Masapila ameiomba Serikali imsaidie kupata gari la kubeba dawa, vyombo vya kunywea, kuni na vyombo vikubwa vya kuchemshia dawa hiyo ili kukabili wingi huo.

Mchungaji Masapila ambaye alistaafu utumishi wa Kanisa mwaka 2001, katika Usharika wa Sonjo, alisema licha ya dawa hiyo kutolewa kwa Sh 500, pia kuna tatizo kubwa la barabara hadi kufika kijijini hapo.

"Tunaomba Serikali kutengeneza barabara kwani wagonjwa wanapata shida sana kufika hapa, nasikia hata nauli zimepanda sana," alisema Masapila.

Gharama za magari zimeendelea kuwa juu kwani hivi sasa wale wanaokwenda kwa kutumia magari ya kitalii wanalazimika kulipa kati ya Sh120,000 na 150,000 na mabasi ni kati ya Sh30,000 hadi 50,000.

Magari hayo sasa yamekuwa yakiondoka Arusha usiku ili kufika Samunge usiku wa manane na hatimaye siku inayofuata wagonjwa wapate dawa.

Kuongezeka kwa kasi kwa watu wanaokwenda kutibiwa kwa mchungaji huyo kumeibua hofu ya kutokea kwa magonjwa ya milipuko kama kipindupindu na kuhara kutokana na kukosekana kwa huduma muhimu za kijamii.

Eneo hilo hivi sasa linakabiliwa na tatizo kubwa la huduma muhimu kama vile majisafi, vyoo, nyumba za kulala na vyakula hivyo wageni hao wengi wakiwa wanakabiliwa na maradhi sugu yakiwemo kansa, kisukari, shinikizo la damu, kifua kikuu na Ukimwi.

Akizungumza na Mwananchi jana, Msaidizi wa Mchungaji huyo, Paulo Dudui alisema maafa makubwa yakiwamo magonjwa ya mlipuko yanaweza kutokea kwa sasa... "Tunaomba (Serikali) msaada wa mahema, vyoo vya muda na huduma muhimu kama mawasiliano kwani hapa kuna watu zaidi ya 6,000 ambao wanalala nje hawana sehemu za kujisaidia, vyakula hakuna na hata mawasiliano hakuna."

Alisema gharama za maisha katika eneo hilo zimepanda kwani bei za vyakula hivi sasa ni kubwa mno akisema hali hiyo ni hatari hasa kwa wagonjwa wanaotolewa hospitali ambao hali zao zinaweza kuwa mbaya hata kabla ya matibabu na hivyo kufariki.

Alisema juzi kuwa Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Elias Wawa Lali aliwatembelea na kujionea hali hiyo na hivyo wana imani suala la msaada litafikishwa katika ngazi za juu.

"Hali ni mbaya sana hapa kama mvua zikinyesha zaidi kunaweza hata kutokea vifo kwani wengi wanaokuja hapa ni wagonjwa," alisema Dudui.

Kuongezeka kwa idadi ya wagonjwa kunatokana na kusambaa kwa taarifa za watu waliopata tiba hiyo na kupona maradhi hayo sugu. Kiongozi mmoja mwandamizi wa CCM Mkoa wa Arusha ambaye hakutaka kutaja jina lake alidai kuwa tangu alipokunywa dawa hiyo, tatizo la sukari ambalo lilikuwa likimsumbua limekwisha.

"Sijui kama nimepona kabisa au la, lakini sasa najisikia vizuri tofauti na mwanzo," alisema kiongozi huyo.

Diwani waViti Maalum (CCM) Wilaya ya Monduli, Dora Kipuyo alidai anamfahamu mgonjwa aliyekuwa na kansa ya mguu ambao ulitakiwa kukatwa, lakini baada ya kupata dawa hiyo sasa vidonda vimekauka.

Baadhi ya watu wenye Virusi Vya Ukimwi (VVU), ambao wamepewa dawa hiyo, licha ya kudai kuwa sasa wana hali nzuri, bado hawajapima kwani wengi waliohojiwa walikuwa hawajatimiza sharti la kukaa siku saba kabla ya kupima ili wajue kama virusi vimekwisha au la.

Mchungaji Masapila alisema dawa hiyo ambayo alioteshwa na Mungu tangu mwaka 1991 na kukumbushwa mwaka 2009, inatokana na maombi na mti wa mgariga ambao unapatikana katika viunga vya Milima ya Sonjo.

Hata hivyo, alisema kupona kwa mgonjwa haraka pia kutokana na imani yake juu ya dawa hiyo ambayo dozi yake ni kikombe kimoja tu kinachonywewa hapo hapo inakotolewa.

Tayari Wizara ya Afya, imekwishatuma wataalam wake kwenda huko kwa ajili ya kufanya uchunguzi wa dawa hiyo.

Source: Globalpublisherstz.com

Loliondo

WAKATI serikali ikijiandaa kutoa majibu ya kisayansi kuhusiana na tiba ya maajabu ya Mchungaji wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Ambilikile Mwasapile (75) mkazi wa Kijiji cha Samunge, Ngorongoro mkoani wa Arusha, maajabu zaidi ya tiba yake yameongezeka.

Akizungumza kwa tabu na gazeti hili kutokana na kuzungukwa na kadamnasi iliyokuwa ikihitaji kuponywa, mchungaji huyo alisema kuwa kabla ya kufika katika kijiji hicho Mei, mwaka 2009, alikuwa akiishi mkoani Manyara akitangaza Injili kama mhubiri wa kawaida na baadaye alistaafu.

Mchungaji Mwasapile ambaye ametazamwa na watu kama ‘Nabii mpya’ amekuwa akitoa tiba hiyo kwa staili ya aina yake ambapo mgonjwa anatakiwa anywe maji yenye dawa hiyo hapo hapo kwa kutumia kikombe kidogo.
Aidha, maajabu mengine ni baadhi ya watu kusema kuwa, mti ambao mchungaji huyo anautumia kutibia unajulikana lakini tatizo bila mkono wake kuchimba mizizi yake hakuna kinachoweza kufanyika.

ALIVYOPATA UTABIBU
Mchungaji Mwasapile anasimulia ilivyokuwa hadi akaoteshwa kuhusu mti huo, anasema:

“Ilikuwa mwaka 1999 nikiwa Babati, kuna siku nikiwa nimelala ilinijia sauti ndotoni. Ikaniamuru kuwa, watu wengi wa Kijiji cha Samunge wanakufa na Ukimwi, kisukari presha na magonjwa mengine mbalimbali.
“Sauti hiyo ikanitaka niwatibu watu hao ili waweze kuendelea na maisha yao kama kawaida. Lakini mimi nilipuuzia sauti hiyo na kuendelea na mambo yangu.
“Hata hivyo, mwaka 2009 sauti hiyo ilinijia tena ndotoni ikinipa maagizo yale yale, lakini safari hii ikanipa onyo kuwa, nisipotimiza agizo hilo nitaadhibiwa.

“Niliamka na kutii, nilikuja hapa kijijini na kwenda hadi kwenye mti nilioelekezwa kuwa ndiyo tiba ya magonjwa yote haya.

“Nilianza kazi hiyo mara moja na tangu siku hiyo umati mkubwa wa watu unamiminika kijijini hapa kadiri wanavyopata habari zangu kutoka kwa watu waliofanikiwa kupona,” alisema mchungaji huyo huku wagonjwa wakiona namchelewesha kutoa tiba kwao.
Hata hivyo, mchungaji huyo alifafanua kuwa, ikitokea amekufa leo, Mungu atamtoa mtu mwingine kufanya kazi hiyo na anaweza akawa si ndugu wala mtoto wake.
Alipoulizwa idadi ya wagonjwa aliowatibu, mchungaji huyo alisema ana uhakika na watu 30,000 huku akisema gharama yake ni shilingi 500 tu kama alivyoagizwa kwenye ndoto. Hivi sasa zaidi ya watu 200,000 wanatibiwa hapo.

MUME NA MKE WAFUMANIANA
Mchungaji huyo anapoendelea na tiba hajui kinachofanyika nje ambako kuna umati wa watu.
Mwandishi wetu alishuhudia watu wawili, mke na mume kila mmoja akimuuliza mwenzake amefikaje kijijini hapo bila kutoa taarifa.
Mwanaume aliyejitambulisha kwa mwandishi wetu kwa jina la Isaya John Jeena alisema alikuwa na mpango wa kwenda kwa mtaalamu huyo kutokana na kusumbuliwa na maradhi ya muda mrefu (hakuyataja).

“Nilikuwa safarini Nairobi, nikapanga nikirudi nije huku, sasa, nashangaa kumkuta mke wangu, kwa nini aje bila kunitaarifu mimi mumewe?” Alihoji Jeena.

VIGOGO NAO WAMO
Tangu aanze kutibu watu, idadi kubwa ya vigogo, wakiwemo wana siasa, maofisa wa serikali na wafanyabiashara wa ndani ya nchi wamekuwa wakimiminika kupata tiba.
Mbali na makundi hayo, baadhi ya wagonjwa waliolazwa katika hospitali mbalimbali za mikoa, ikiwemo Kilimanjaro Christian Medical Center (KCMC) ya mjini Moshi, wamekuwa wakiomba ruhusa kutoka wengine wakitumia njia ya kutoroka ili wakatibiwe kwa mchungaji huyo.

Kwa sasa katika Kijiji cha Samunge, watu waliofurika ni wa kutoka Mikoa ya Arusha, Kilimanjaro, Singida, Mbeya, Manyara , Dar es Salaam na nchi jirani za Kenya na Uganda.

Magari mengi ya kifahari ya vigogo yalionekana mwishoni mwa wiki iliyopita yakiwa yamezungukwa na askari wa FFU wakishirikiana na mgambo kuhakikisha kuwa hakuna mwandishi wa habari ama mtu yeyote atakayeruhusiwa kupiga picha eneo hilo.

Mabasi kutoka Dar, Arusha na Moshi yamekuwa yakianzisha ‘ruti’ za kwenda Loliondo moja kwa moja kutoka katika miji hiyo.
Hata hivyo, kutokana na idadi kubwa ya watu wanaokwenda eneo hilo huduma ya vyakula imepanda ambapo wageni wanaofika hapo wamekuwa wakilazimika kubeba vyakula vyao baada ya kujikuta wakiuziwa sahani moja ya chakula kwa shilingi kati ya 5,000 na 10,000.
Awali kulikuwa na watu walikuwa wakichinja mbuzi 50,000 kwa siku lakini sasa wamezuiliwa kutoa huduma hiyo.

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa, katika eneo hilo hakuna idadi kubwa ya vyoo vya kujisaidia, hivyo watu kujikuta wakienda vichakani.

Aidha, imebainika kuwa, hata ‘madada poa’ wanaofanya biashara ya kuuza miili katika maeneo mbalimbali ya starehe mjini Arusha, nao wamepungua baada ya wengi wao kutimkia kwa mchungaji huyo kutokana na kuamini wana maambukizi ya Virusi vya Ukimwi.
Usafiri wa kutoka mjini Arusha hadi Samunge umepanda ghafla kutoka shilingi 35,000 kwenda na kurudi hadi kufikia shilingi 150,000 kwa magari yanayomudu kufika huko kwani barabara ni mbovu.

Ingawa hakuna taarifa rasmi zilizothibitisha kuwa mgonjwa wa Ukimwi amepona lakini Lilian John (30) mkazi wa kijiji hicho alisema kuwa aligundua ana maambukizi ya Ukimwi mwaka 2006 baada ya kufiwa na mume na mwanaye.

Alisema mwaka 2009 alibahatika kuonana na mchungaji huyo wakati huo alikuwa siyo maarufu na kumpatia dawa hiyo.

Baada ya kuitumia kwa wiki mbili alikwenda kupima katika Hospitali Teule ya Wasso ambapo madaktari walithibitisha kuwa, hana Virusi vya Ukimwi.

SERIKALI INASEMAJE?
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Isidori Shirima amesema serikali haioni sababu ya kuzuia watu kupata tiba za mchungaji huyo kama hazina madhara kwa afya zao.
Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Blandina Nyoni amesema wizara yake imeiagiza ofisi ya mganga mkuu wa mkoa ifanye utafiti wa kimaabara juu ya dawa hiyo kwa kushirikiana na Taasisi ya Taifa ya Uchunguzi wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) ili kubaini ukweli wa kisayansi na watatoa taarifa uchunguzi ukikamilika.

Source: Globalpublisherstz.com