Thursday, February 26, 2009

Smart card and number 666

Ushawahi kusikia kuhusu smart card ?
Ushawahi kusikia kuhusu biochip ?
Ushawahi kusikia kuhusu cashless society ?
Ushawahi kusikia kuhusu integreted computer system?
Ushawahi kusikia kuhusu New World Order ?
Wasikilize wataalamu wa DigitalBrain wakifafanua kuhusu mada hii tata na ya muhimu sana katika siku hizi za mwisho.
sikia hapa live www.digitalbraintz.com

Wednesday, February 25, 2009

JE UNAFAHAMU FAIDA ILIYOPO KATIKA KUIMBA NYIMBO ZA ROHONI?--2

KUIMBA NA KUSIFU –SILAHA KUBWA KATIKA VITA.

Ndugu katika Kristo, Nakusalimu katika Jina lipitalo majina yote, Jina ambalo kwalo sisi wanadamu wote tunaokolewa kutoka dhambini, Jina linalotubariki, Jina linalotuweka huru, Jina zuri la Yesu Kristo. Nakutakia neema na amani tele katika kumjua Mungu na Yesu Bwana wetu. (1Peter 1:2)

Wiki iliyopita kwa msaada wa Roho Mtakatifu tulijifunza sehemu ya kwanza ya somo hili, linalotuonesha umuhimu wa sisi tumwaminio Kristo kuimba nyimbo za rohoni. Ninaamini Roho Mtakatifu alikuwa juu yako kukufundisha na ukaelewa vizuri, ninanamshukuru Yeye hata kwa ajili ya wale walionitumia shuhuda zao. Kati ya hao, ndugu mmoja alinieleza kuwa kuna wakati alikuwa kiimba nyimbo za Tenzi za Rohoni akiwa anaishi katika nyumba za kupanga, na ikawa inatokea kuwa kuna wakati akiwa anaimba, mapepo yanawapagawa na kuwatoka baadhi ya wapangaji wengine, pamoja na kuwa alipewa notice kwenye nyumba hizo.

Leo tunaendelea na sehemu hii ya pili na ya mwisho ya somo hili, na leo tuangalia Faida za kuimba nyimbo za sifa&kushukuru mara tuwapo katika mapito magumu.

Leo tutazama vita ya ajabu kama ilivyorekodiwa katika kitabu cha 2 Mambo ya Nyakati sura ya 20. Ili kukusaidia wewe kuelewa vizuri zaidi habari hii ninakupa shauri, pata muda na usome vizuri sura nzima hii ya 20, mimi hapa nitataja mistari michache tuu.

Habari hii inaanza katika mstari wa kwanza kabisa, ambapo tunaona kuwa mataifa matatu yalitoka na kwenda kujipanga kuwavamia wana wa Israeli (kabila lile la Yuda) katika nchi yao waliyopewa kukaa na Mungu Baba. Ndipo mtu mmoja akatoka na kwenda kumpa mfalme wa Israel (Yehoshafati) habari hizi za uvamizi. Hizi zilikuwa ni habari za kusikitisha na kuogopesha sana, kwa ilikuwa ni mataifa matatu yaliyojiandaa yanawavamia wana wa Israeli, wale wa Yuda, taifa moja.

Biblia inatuambia wazi kabisa katika mstari wa tatu kuwa hata Yehoshafati mwenyewe aliogopa, lakini kulikuwa na jambo moja zuri katika kuogopa kwake- yeye alikwenda kumwomba Mungu Baba juu ya uvamizi huu na akatangaza kufunga katika nchi nzima (ingekuwa baraka namna gani kama leo Taifa zima la Tanzania, au angalau hata kanisa tuu tukapanga kufunga siku Fulani kwa ajli ya jambo Fulani katika nchi yetu?) na tunaona kuwa walitoka katika miji ya Yuda na wakakusanyika pamoja kumwomba Mungu Baba kwa ajili ya hili.

Tunaona kuwa baada ya kukutana mbele za mfalme, mfalme aliomba maombi ambayo yalifanya hata wana wa Israeli wakatiwa moyo. Kisha Roho Mtakatifu akashuka juu ya nabii mmoja naye akasimama na kuwaeleza watu wote kuwa wasiogope kwani Baba Mungu anasema kuwa vita sio vyao bali ni vya Bwana(mstari wa 15)-{Ni vyema na wewe ukajisemea na kuamini hili kila mara unapokutana na majaribu mbalimbali katika maisha yako}. Kwa maana nyingine, Mungu alikuwa amekuja kuwasaidia katika vita vile. Kisha yule nabii akaendelea kuwaambia kuwa hawatahitaji kupigana vile vita, bali wao wafike tuu katika uwanja ule wa mapambano na waoune wokovu wa Bwana. Wakamwabudu Bwana (inawezekana waliimba nyimbo za kuabudu) na wakalala usiku ule kwa amani.
Wakaamka asubuhi iliyofuata, ambayo ilikuwa ndiyo siku ya kwenda vitani, sasa kwa namna tuliyozoea sisi, tungejipanga kwa kila mtu kupewa silaha na kufundishwa namna ya kupigana-hata kama tumeshaambiwa kuwa vita ni vya Bwana na sio vyetu, lakini alichofanya mfalme Yehoshafati ni tofauti kabisa na ndio hasa ninataka ujifunze wiki hii nzima.

Biblia inatuambia kuanzia mstari wa 21 kuwa, mfalme aliamka asubuhi ili kuongea na watu juu ya vita vilivyo mbele yao, na badala ya kuwapanga namna ya kupigana, yeye aliwapanga watu kwa ajili ya kuimba nyimbo za kumsifu Bwana kwa uzuri wa utakatifu wake. Tena akawaambia watangulie mbele ya jeshi lao wakiimba na kusema “Msifuni Bwana kwa maana fadhili zake zadumu milele”

Mstari wa 22 unasema “ Na walipoanza kuimba na kusifu, Bwana akaweka waviziao kinyume cha wana wa Amoni,Moabu na mlima Seiri waliokuja kupigana kinyume cha Yuda; nao wakauawa” Biblia haiweki wazi kuwa hawa “waviziao” ni kina nani lakini inavyoonesha, hawa ni malaika ambao Bwana aliwateremsha kuja kuwasaidia Yuda. Na kilichotokea ni wale wa mataifa waliokuja kuwashambulia wana wa Yuda walianza kupigana wao kwa wao hadi wakamalizana. Wana wa Yuda walipofika hapo walipo, walikuta maiti zao tuu, maadui zao wote walikufa! Huu ni ushindi mkubwa sana ambao Bwana aliwapatia bila nguvu zao hata kidogo na tunaambiwa kuwa wana wa Yuda walitumia siku tatu kukusanya nyara (mali) walizokuwa nazo wale maadui zao na kisha wakamshukuru Bwana.
Hebu utazame tena huo mstari wa 22. Utaona kuwa umeanza na maneno “na walipoanza kuimba na kusifu, Bwana akaweka waviziao………..” Maana ya haya maneno ni nini katika mstari huu?
Maana yake ni kwamba, Bwana hakuanza kuwapigania wao ila mpaka pale walipanza kuimba na kusifu. Yaani muda wote Bwana alikuwa kimya anawatazama watafanyaje, walipoanza kuimba na kusifu ndio akawapigania. Tupo pamoja?

Je unajifunza nini hapa? Hii ina maana kuwa wasingeanza kuimba na kusifu, Bwana angekaa kimya kabisa, nap engine wangeamua kupigana vita vile kwa nguvu za jeshi lao na wangeshindwa kwa sababu huo ulikuwa siyo mpango wa Mungu Baba kuwasaidia (sio kila mpango ni mpango wa Bwana kukusaidia pale upatapo shida). Hivyo Bwana alikaa kimya hadi pale walipoanza kuimba na kusifu.

Sasa nataka ujiulize, ni kwa nini Bwana awasubiri hadi waimbe na kusifu? Kwa nini sio hadi waombe na kufunga siku kadhaa? Kwanini kuimba?
Ukijiuliza swali hili utaona tena faida nyingine ya kumsifu Bwana pale unapopita katika magumu ya ulimwengu huu.

Sababu iliyopo ni kwa kuwa “Uimbaji ni sauti ya Imani” (“Praise is the voice of faith”). Yaani, unapoimba wimbo Fulani katika Roho, kwa kumaanisha, unaonesha imani iliyo ndani ya moyo wako kwa Bwana. Baada ya kumwomba Baba Mungu juu ya jambo fualani, je unaamini kuwa atakufanyia kama ulivyomwomba? Je, unaioneshaje imani yako? Njia mojawapo ya kuonesha imani ya mtu anapopita katika hali Fulani ngumu ni kwa kusikiliza maneno anayosema juu ya hali ile ngumu. Ukimsikia anasema maneno ya kukata tamaa, kuwa haamini kuwa Bwana atamsaidia hapo, basi ujue imani yake imekufa (na hiyo ni hali ya hatari) lakini ukimsikia anakiri ushindi kutoka kwa Bwana hata kama hali ni mbaya kiasi gani, basi mtu huyu anayo imani iliyo hai na Bwana atamsaidia mara moja.

Kwahiyo unapopita katika majaribu au hali yoyote ngumu usiyoipenda, ni vyema kumwomba Bwana kwa Jina la Yesu, na baada ya kumwomba, Atataka kuona imani yako, kwa hiyo anza kuimba nyimbo kadha wa kadha za kumsifu Bwana, uziimbe kwa kumaanisha na moyoni mwako ukimsifu Bwana kwa kukusaidia katika hali ngumu unayopitia, maana hiyo ndiyo imani yako. Ukifanya hivyo, wewe utakuwa ni sawa na wale wana wa Yuda walipoanza kuimba na kusifu, na Bwana akaja na kuwasaidia. Bwana atakusaidia na wewe. Na hilo ndilo kusudi la Roho Mtakatifu kukuletea ndani ya moyo wako nyimbo za kusifu kama tulivyoona kwenye sehemu ya kwanza ya somo hili.

Ninaamini kuwa umeona faida nzuri zilizo katika kumwimbia Bwana nyimbo katika Roho, kwa kumaanisha. Ukijisomea Biblia zaidi pia unaweza ukaona namna huduma ya uimbaji ilivyo ya muhimu sana katika kuujenga mwili wa Kristo. Na ninaamini kuwa utabarikiwa sana ukiyaweka haya katika matendo.
Watu wote tumshukuru na kumsifu Mungu Baba kwa kutuletea somo hili kwa wakati huu, na hapa ikiwa ni mwisho wa somo hili, Amen.
********************

SEMINA YA MWAKASEGE ARUSHA
Tangazo: Kwa wale wakazi wa jiji la Arusha, tunamshukuru Mungu kwa kuwa semina ya Neno la Mungu ya Mwalimu Christopher Mwakasege imeanza hapa Arusha tarehe 22 mwezi huu na itamalizika tarehe 1 mwezi wa tatu. Kwa wale wakazi wa Arusha na maeneo ya jirani, huu ni wakati wa kwenda kupata maarifa ya Neno la Mungu pale. Lakini pia kwa wale waishio nje ya Arusha na wangependa kupata mafundisho ya semina hii yake katika kanda za redio, kanda za video(VHS), Audio CDs, au DVD basi wawasiliane nami ( savedlema2 at yahoo dot com) ili nione namna naweza kuwasaidia kwa kuwatumia.

****************
Je una ushuhuda wowote wa matendo ambayo Bwana amekufanyia katika maisha yako au familia yako na ungependa watu wengine wauosome na imani yao kwa Bwana iongezeke? Kama ndivyo basi ingia katika website yangu
www.lema.or.tz na kisha click ukurasa wa “Shuhuda” na uandike ushuhuda wako hapo.

********************
Tuzidi kuombeana tafadhali,
Frank Lema
www.lema.or.tz
Arusha.

Thursday, February 19, 2009

JE UNAUFAHAMU UMUHIMU AU FAIDA YA KUIMBA NYIMBO ZA ROHONI?


Bwana Yesu Kristo asifiwe!

“Nakutakia neema na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na Bwana wetu Yesu Kristo.”(1Kor1:4)

JE UNAUFAHAMU UMUHIMU AU FAIDA YA KUIMBA NYIMBO ZA ROHONI?

Bwana Yesu asifiwe tena! Ninamshukuru Mungu,Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo kwa wema wake ulio mkuu sana kiasi kisichoweza kuelezeka kwa namna ya kibinadamu, kwa kunilinda mimi na wewe pia mpaka kufikia hapa, tunajua kuwa hii ni neema tunayotakiwa kumshukuru Mungu kwayo.

Ni muda mrefu umepita tangu nikuletee ujumbe wa Neno la Mungu kwa njia hii(kwa wale waliokwishajiunga na huduma hii tayari), na kama wewe ndio umejiunga na huduma hii karibuni, basi karibu na ubarikiwe.

Leo ninakuletea kwa uwezo wa Roho Mtakatifu ujumbe huu unaosema “Je, unaufahamu umuhimu wa kuimba nyimbo za rohoni?”

Kuna faida kubwa sana tunayoipata pale tunapoimba nyimbo mbalimbali za rohoni katika Kristo Yesu. Ninaposema kuimba hapa, siyo lazima uwe umepewa huduma na karama ya uimbaji kama tunavyowaona waimbaji wengi wakiimba na kurekodi nyimbo zao, hapana. Kila mtu aliyeokoka amepewa ndani yake aina Fulani ya uimbaji, hata kama siyo karama yake, japokuwa unaweza kuimba kidogo tuu, lakini Baba Mungu ndiye ameweka hicho kitu ndani ya kila aliyeokoka. Kwanini Baba Mungu ametupa aina hii ya uimbaji hata kwa watu ambao huduma yao wanayomtumikia Mungu kwayo siyo ya uimbaji? Hii ina maana zipo faida za kipawa hiki Mungu alichoweka ndani yetu na inapaswa tukitambue na tukitumie vyema.

Kwanza hebu soma na UITAFAKARI mistari hii hapa chini:

“Je, pana mtu yeyote miongoni mwenu aliye na shida? Anapaswa kusali. Je, yuko mwenye furaha? Anapaswa kuimba nyimbo za sifa”.(Yakobo 5:13)

“Ujumbe wa Kristo ukae ndani yenu pamoja na utajiri wake wote. Fundishaneni na kushauriana kwa hekima yote. Imbeni zaburi, nyimbo na tenzi za kiroho; mwimbieni Mungu mioyoni mwenu kwa shukrani.”-(Kolosai 3:16)

1Samweli 16:23 : “Ikawa, ile roho mbaya kutoka kwa Mungu ilipomjilia Sauli, ndipo Daudi akakishika kinubi, akakipiga kwa mkono wake, naye Sauli akaburudishwa na ile roho mbaya ikamwacha”


Bila shaka baada ya kuitafakari mistari hiyo hapa juu umeanza kupata picha kidogo juu ya jambo hili.
Mungu ametupa aina hii ya uimbaji ndani yetu kwa ajili ya kutusaidia katika maeneo mbalimbali tunayopitia hapa duniani.

Unaona katika mstari ule wa Yakobo 5:16, Roho Mtakatifu anasema kuwa kama mtu ana shida basi anapaswa kuomba, kisha akasema kuwa, kama mtu ana furaha basi anapaswa kuimba nyimbo za sifa. Bila shaka nyimbo hizi kwa ajili ya kumsifu na kumshukuru Mungu kwa jambo alilolifanya hata ukawa na furaha. Je, unafikiri Roho Mtakatifu ametoa agizo hili bure? La Hasha! Lazima jambo hili ni la muhimu sana ndio maana ametuagiza tufanye hivyo.
Naandika waraka huu wa leo kukuhimiza kuhusu kuimba nyimbo za rohoni kwa Bwana. Wakati wowote unapokuwa mahali na ukaona tuu kuwa ndani ya moyo wako unajisikia furaha, basi pata muda mahali wewe mwenyewe au na watu wengine na uimbe nyimbo zozote utakazokuwa nazo za kumsifu Baba Mungu na utaona matunda yake, Mungu atafurahi na ataendelea kukupa hiyo furaha zaidi.

Ukitazama ule mstari wa kwenye kitabu cha Samweli 16:23 unaona kuwa mfalme Sauli alijiwa na roho mbaya iliyomsumbua, na ukisoma mistari inayotangulia utaona kuwa, Sauli alipoona tatizo hili, hakumwita kuhani aje kumwombea, bali baada ya kushauriwa, aliagiza aletwe mtu wa kumpigia kinubi pale roho ile itakapomjia, na akaletwa Daudi. Na ikawa kuwa kila roho ile ilipomjia, Daudi alikipiga kinubi chake na roho mbaya ikamwacha Sauli. Hebu tazama tofauti ya jambo hili lililotokea hapa na lile liliagizwa katika mstari ule wa Yakobo! Kwa waraka wa Yakobo tunaagizwa kuomba pale tunapopatwa na jambo lisilo jema, lakini hapa kwa Samweli, Sauli ameshauriwa kupata mtu wa kumwimbia!

Ni wazi kuwa, kuna mahali Mungu Baba ataamua kukusaidia kwa kukuongoza kuomba, na mahali pengine Atakuongoza kuimba tuu nyimbo katika Roho. Unachotakiwa ni kusikiliza ndani ya moyo wako unasukumwa kufanya kipi.

Unapoimba nyimbo za kiroho mahali popote kuna mambo mazuri yanatokea. Nafsi yako inaponywa majeraha yoyote uliyoyapata, iwe ni kwa kuonewa, kutukanwa au majeraha yoyote yale ya kwenye nafsi. Pia unajazwa nguvu za Roho Mtakatifu ndani yako kwa namna ya ajabu.

Siku moja kuanzia mida ya mchana hivi, niliona kuwa kuna wimbo Fulani wa kwenye kitabu cha Tenzi za Rohoni unakuja sana moyoni mwangu bila hata kusikia mtu akiuimba popote japokuwa hata sifahamu beti zake vizuri. Hali hii iliendelea kwa siku nzima, wimbo huo ulikaa sana moyoni mwangu na kila mara nilipokuwa free nilijikuta tuu naanza kuuimba kidogo. Nikapanga kuwa baadaye nitauimba. Jioni niliporudi kupumzika, nilichukua kitabu changu cha Tenzi za Rohoni na nikaanza kuuimba huo wimbo. Nilipofika katikati ya ule wimbo, ghafla niliona nimeteremkiwa na kujazwa nguvu za Roho Mtakatifu kwa namna niliyoishangaa sana, kwani hata sikuomba hata kidogo kabla ya tukio hili. Baada ya hapo ndio nikagundua ni nini maana yake mtu anapokuwa katika shughuli zake na ghafla anasikia ndani yake wimbo Fulani umekuja hata kama haufahamu wote. Kwa hiyo tangu hapo mimi huwa karibu na vitabu vyangu viwili vya nyimbo (Tenzi za Rohoni na Holiness Song Book) na kila nisikiapo Roho Mtakatifu ameweka wimbo Fulani ndani yangu, ninahakikisha kuwa nimepata muda mzuri wa kuuuimba mimi mwenyewe au na wenzangu, na mara kwa mara nipatapo nafasi hukaa na kuimba nyimbo kadhaa kwenye vitabu hivi. Kama naona sifahamu sauti ya wimbo Fulani basi huwa natafuta mtu anayeujua namwomba tuuimbe, au natafuta ala (Midi files) za huo wimbo na kuimba kwa kuzifuatia. Na baada ya kuuimba huwa ninajua kwa hakika kabisa kuwa kuna kitu Mungu amenifanyia wakati nikiuuimba. Yaweza kuwa ni moyo wangu umeponywa, maombi yangu yamejibiwa au imani yangu imeongezwa wakati nilipoimba ule wimbo. Sasa utaona ni kwa nini Biblia inatushauri tufarijiane kwa nyimbo hizi hata wakati wa maombolezo, mioyo yetu inaponywa na tunaongezewa imani.

Wakati mwingine unapomwomba Mungu Baba jambo, anakutaka uonyeshe imani kuwa unaamini kuwa kile ulichoomba ni chako tayari (kama Biblia isemavyo) na ili kukusaidia uonyeshe imani yako, anakuwekea ndani ya moyo wako wimbo wa kumshukuru Mungu Baba, hata kama wimbo wenyewe hujawahi kuuimba miaka kadhaa, na utajikuta tuu unataka kuiimba na utashangaa pia kuwa wala hakuna mtu yeyote aliyekutajia huo wimbo, na wala hujamsikia mtu akiuimba huo wimbo.


Je, na wewe umeshakutana na jambo kama hili? Ulichukua hatua gani? Watu wengi hujikuta wanapuuzia tuu na kusema “Ah! Huu wimbo umetoka wapi tena saa hizi na mimi nipo na kazi zangu?” Nimekuletea waraka huu kwa Roho Mtakatifu ili kukusaidia, kuanzia sasa unapoona hali ya namna hii, hakikisha kuwa unapata muda mzuri uliotulia na ukae na kuziimba nyimbo hizi, ni za muhimu sana. Ninakupa shauri sasa, nunua vitabu vyako vya nyimbo (kama Tenzi za Rohoni) ukae nacho pale ulipo, na unapopata muda, tafuta wimbo mmojawapo na uuimbe, baada ya muda mfupi utaona faida yake njema. Kama unafamilia yako, tengeni muda wa kuomba kila siku usiku (kwa mfano) kabla ya kulala, na kabla ya kuomba, changueni nyimbo chache za rohoni kutoka kwenye vitabu mlivyonavyo na mziimbe wote kwa pamoja. Baada ya muda mfupi mtagundua kuwa upendo na mshikamano ndani ya familia (au kundi lolote) unaongezeka kwa namna msiyoijua na Mungu anajibu maombi yetu kwa namna mnayofurahi zaidi.

Huu ndio ujumbe Bwana aliouweka moyoni mwangu siku hii ya leo kwa ajili yako na ninaamini kuwa utafanyika baraka kubwa sana kwako pale utakapouweka katika matendo, na hayo ndio maombi yangu kwa Baba Mungu.

“….Je yuko mwenye furaha? Anapaswa kuimba nyimbo za sifa”

Mungu Baba akubariki na tuzidi kuombeana daima.

Ni mimi katika Kristo,
FRANK LEMA.
www.lema.or.tz
Arusha Tanzania.


// Kupokea ujumbe huu kwa email jiunge na mailing lists kwa kutembelea www.lema.or.tz //

Wednesday, February 18, 2009

Mchungaji Auwawa kwa baada ya kufumaniwa

MCHUNGAJI wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Mtaa wa Manundu mjini hapa, Bw. Ernest Mngazija (52) ameuawa kwa kuchomwa kisu baada ya kufumaniwa na mke wa mtu akifanya naye mapenzi ndani ya nyumba yao. Tukio hilo lilitokea juzi saa 2. 30 usiku baada ya Mchungaji huyo kukutwa katika nyumba yenye namba HMK/MT/86 iliyopo mtaa wa Mtonga nje kidogo ya mji wa Korogwe. Mchungaji huyo aliyeacha mke na watoto zaidi ya watano, alikutwa na Bi. Happy Temu (19) ambaye ni mke wa Bw. Mandia. Mwandishi wa habari hizi alipofika katika eneo la tukio jana alishuhudia michirizi ya damu kutoka nyumba aliyofumaniwa mchungaji huyo hadi sehemu aliyoangukia kiasi cha mita 100 baada ya kukosa nguvu kutokana na damu kumtoka nyingi. Akizungumzia tukio hilo, Bw. Herman Kiluu ambaye ni Balozi wa mtaa wa Mtonga Juu (Meco) alisema, Mchungaji huyo alikutwa akifanya mapenzi na mke huyo nyakati za usiku. Alisema baada ya kijana huyo kumkuta mchungaji alikwenda kutoa taarifa kwa Mwenyekiti wa Mtaa huo, Bw.Hassan Mndolwa 'Segere Kuu'ambaye naye alifika nyumbani kwake ambapo walivunja mlango wa nyumba hiyo baada ya mke kukataa kufungua na hivyo kuingia ndani kujua kulikoni. "Mchungaji alipotoka alikatwa kisu cha shingo na Mandia, akakatwa tena huku akitafuta njia za kukimbia na vijana walikuwa wakipiga kelele za mwizi," alisema Bw. Kiluu. Alisema hata hivyo, baada ya Mchungaji kukatwa visu vingi alikosa nguvu na kuanguka jirani na nyumba yake ambapo walimpeleka Hospitali ya Magunga kupitia Polisi lakini alifariki akiwa njiani kabla ya kufikishwa hospitali kutibiwa. Tukio hilo limeibua maswali mengi kwani wiki iliyopita, Mchungaji huyo aliongoza misa ya marehemu Salmin Karata ambaye alikuwa dereva wa World Vision aliyekufa kwa ajali ambapokatika mahubiri yake alisema watu wajiandae na kifo. "Leo hii Salmin kesho mimi au wewe," alikaririwa akisema. Kamanda wa Polisi mkoa wa Tanga, Bw. Sirro Nyakoro alithibitisha kutokea kwa mauaji hayo na kusema mtuhumiwa anasakwa na Polisi kwani alikimbia baada ya mauaji hayo. Alisema Happy alihojiwa na Polisi na kuachiwa na atakuwa shahidi kesi hiyo itakapoanza kusikilizwa. Shahidi mwingine atakuwa Balozi aliyeitwa na mtuhumiwa kushuhudia ugoni. Kamanda alisema, marehemu alichomwa visu mara nne katika sehemu mbalimbali za mwili na kutokwa damu nyingi na alikutwa uchi wa mnyama akivaa chupi mlango ulipovunjwa. Alipoulizwa walijiridhishaje Mchungaji alikuwa amefanya mapenzi na Bi. Happy Kamanda alisema 'mtu amekutwa uchi wa mnyama anavaa chupi maana yake alikuwa anafanya nini".

Mchungaji ‘akutwa’ na viungo vya albino

Mchungaji wa Kanisa la Pentecoste lililopo Idiwili Kata ya Iyula, wilayani Mbozi anashikiliwa na Polisi kwa tuhuma za kukutwa na mabaki ya mwili wa binadamu yaliyokuwa yakiuzwa Sh milioni 30. Cosmas Mwasenga (39) alikamatwa Februari 13 mwaka huu akiwa na Luseshelo Mwashilindi ambaye inadaiwa alikuwa ameyahifadhi nyumbani kwake mabaki hayo. Mabaki hayo ambayo Polisi inahisi kuwa ni ya albino, ni vipande vinne vinavyosadikiwa kuwa sehemu ya mikono. Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya, Zelothe Stephen alisema leo kuwa watuhumiwa hao walikamatwa katika eneo la Mlowo, Mbozi. Akizungumzia tukio hilo, Kamanda Zelothe alisema Februari 12 mwaka huu, polisi walipata taarifa kuwa kuna kikundi cha watu Mlowo, wana vipande vya mabaki ya mwili wa mwanadamu vinavyosadikiwa kuwa ni mabaki ya mwili wa albino. Alisema taarifa hizo zilidai kuwa kikundi hicho kilikuwa kinatafuta wateja ili kuwauzia vipande hivyo na kwamba watu waliokuwa wanatafuta wateja waligawanyika katika Wilaya ya Mbozi na baadhi ya mitaa ya Jiji la Mbeya. “Tuliweka mtego na kukutana na watu hao ambao walisema wanauza viungo vya ‘kunguru mweupe’ wakimaanisha albino, ambapo walikubaliana na kukutana na Mwashilindi ambaye alikuwa anahifadhi viungo na kufikia makubaliano ya kuvinunua kwa Sh milioni 30,” alisema. Alisema Februari 13, taratibu za kupata kiasi hicho cha fedha zilikamilika na walipofika kwa Mwashilindi alitoka akiwa na vipande vinne vya mabaki ya binadamu vikiwa vimefungwa katika karatasi, na Polisi wakamkamata. “Baada ya kupekua katika nyumba ya Mwashilindi tulifanikiwa kupata dawa za binadamu, maji ya kuchanganya na dawa na koti jeusi mali ya Mchungaji Mwasenga,” alisema. Aliongeza kuwa watuhumiwa wote wawili wanashikiliwa na watafikishwa mahakamani baada ya uchunguzi kukamilika. Kamanda Zelothe alisisitiza umuhimu wa wananchi kutoa taarifa Polisi na kusema kwa kufanya hivyo, ndipo vitendo vya mauaji ya albino vitapungua. “Tunapenda kuwaomba wananchi waendelee kutoa taarifa za siri kwa viongozi wa juu, ili ziweze kufanyiwa kazi haraka,” alisema.

Friday, February 6, 2009

Mchungaji afungwa kwa kukataa kuapa mahakamani

Mchungaji wa Kanisa la EAGT lillilopo mtaa wa Ichenjezya mjini Vwawa wilayani Mbozi mkoani Mbeya Simon Kitwike (48) jana alijikuta akihukumiwa kifungo cha miezi sita gerezani, baada ya kudharau mahakama kwa kukataa kuapa ili atoe ushahidi kutokana na imani ya Dini.Mchungaji huyo aliyevunjiwa nyumba yake mwishoni mwa mwaka jana na kuibiwa mali kadhaa za nyumbani kwake alifika katika mahakama ya wilaya ya Mbozi ili kutoa ushahidi wake, lakini alikataa kuapa kabla ya kutoa ushahidi wake akidai ni dhambi.Hakimu wa mahakama ya wilaya Kajanja Nyasige alimwamuru asome kifungu katika Biblia kinachomtaka asiape mahakamani, ndipo mchungaji huyo alifungua Biblia na kusoma kitabu cha Mathayo 5: 35 kuwa ndicho kinachompa msimamo huo.Baada ya kusoma kifungu hicho Hakimu Nyasige alimuuliza tena mshitakiwa (shahidi) kama atakuwa tayari kuapa ili aweze kuendelea na kutoa ushahidi wake mahakamani, hata hivyo mshitakiwa huyo aliendelea kubaki na msimamo wake wa kukataa kuapa.Ndipo Hakimu huyo alimsomea kifungu cha sheria na 198 (1) kama ilivyorekebishwa mwaka 2002 kinachokataza mtu kudharau Mahakama na kuwa kuendelea kukataa kuapa ni kuvunja sheria na hivyo anatenda kosa la jinai.Hata hivyo hakimu Nyasige aliendelea kumvumilia mchungaji huyo ili aweze kubadili msimamo wake kwa kumwamuru asome Biblia hiyo tena Waraka wa Mtume Paulo kwa Warumi 13:1- 5, shahidi huyo alisoma kifungu hicho mbele ya mahakama, lakini alipoulizwa kama amebadili msimamo wake alijibu kuwa hawezi kubadili msimamo wake, kwa aya hiyo ya waraka na akasisitiza kuwa msimamo upo pale pale.Hakimu Nyasige alilazimika kumsomea hukumu na kumtia hatiani kutokana na kosa la kuidharau mahakama, hivyo anamhukumu kwenda jera miezi sita na kuwa atatakiwa kuja kutoa ushahidi wake kwa kesi ya msingi Marchi 2, mwaka huu.Mwandishi wa habari hizi alimhoji Mchungaji mwandamizi wa Kanisa hilo aliyejitaja kwa jina moja la Mwakasaka ambaye alisema amesikitishwa na hukumu hiyo na akadai kuwa mchungaji wake alielewa vibaya vifungu vya biblia vinavyozungumzia viapo.Naye Mchungaji Erasto Makalla wa kanisa la Pentekoste alieleza kusikitishwa kwake na hatua hiyo ya mchungaji kupingana na mamlaka ya serikali na akasema kuna haja ya kuwafanyia semina wachungaji ili waelewe taratibu za serikali.Matukio ya upinzani yamekuwa yakijitokeza mara kwa mara wilayani hapa ambapo mwaka juzi waumini wa madhehebu ya Mashahidi wa Jehova walikuwa kwenye mgogoro na serikali baada ya kukataza wanafunzi wasiimbe wimbo wa taifa na kuheshimu bendera.

Kikwete na UDOM

Rais Jakaya Mrisho Kikwete ametangaza kuwa amefanya uamuzi kuwa makao makuu ya Serikali mjini Dodoma sasa yatajengwa katika eneo la Chamwino, baada ya eneo lililokuwa limetengwa awali kwa ujenzi huo katika eneo la Chimwaga, kutolewa kwa ajili ya ujenzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), chuo kikubwa zaidi cha umma nchini.
Rais Kikwete pia ameutaka uongozi wa chuo hicho cha UDOM kuelekeza nguvu zaidi katika kufundisha wataalam zaidi wa shahada kubwa zaidi za Uzamili na Uzamivu, badala ya kushikilia kufundisha watu kwa ajili ya kupata shahada la kwanza tu.
Rais Kikwete ameelekeza hayo wakati alipotembelea UDOM, ili kujionea maendeleo ya wa chuo hicho, ikiwa ni mara yake ya kwanza kutembelea chuo hicho tokea alipokwenda kukagua ujenzi wa chuo hicho Agosti 2, 2007.Akizungumza na jumuia ya wanachuo baada kumaliza kutembelea chuo hicho na kukagua ujenzi wake, Rais Kikwete amesema kuwa ameamua kuwa sasa makao makuu ya Serikali yatajengwa katika eneo linalozunguka Ikulu Ndogo ya Chamwino, baada ya kuwa ametoa eneo la awali la ujenzi wa makao makuu hayo kwa ujenzi wa UDOM.
“Kuna sababu mbili za kufanya hivyo. Moja ni kwamba eneo hili sasa tumelitokea kwa ajili ya ujenzi wa chuo hiki maridadi na cha kupendekeza kabisa. Hata kabla ya ujenzi kumalizika, nyie mnajionea kinachovutia,” amesema Rais Kikwete na kuongeza:
“ Pili ni kwamba Rais hawezi kufanya kazi ya kusafiri mwendo mrefu kiasi hiki kati ya makazi yake ya Chamwino na ofisi yake kwenye eneo hilo la Chimwaga,” Rais Kikwete amewaambia wanajumuia hao.
Inakisiwa kuwa kuna umbali wa kiasi cha kilomita 35 kutoka Chamwino kwenda mjini Dodoma. Hivyo, safari ya kutoka Chamwino kwenda Chimwaga na kurudi ni kiasi cha kilomita 70.
Rais Kikwete amewaambia wanajumuia hao wa UDOM kuwa ameshangazwa kweli kweli na hatua ya ujenzi wa Chuo hiki. “Nimepata faraja kubwa moyoni mwangu. Naamini kuwa baada ya ujenzi, eneo hili litakuwa moja ya maeneo ya kuvutia zaidi nchini, na wala sisemi maeneo ya vyuo viku, bali majengo yote.”
Rais Kikwete pia amewaelezea wanajumuia hiyo jinsi wazo la kuanzisha chuo hicho lilivyozaliwa, kwa sababu uamuzi wa kuanzisha chuo hicho ulikuwa uamuzi binafsi wa Rais Kikwete, na wala hilo halikuwa sehemu ya Ilani ya Uchaguzi Mkuu wa CCM, mwaka 2005.
Amesema kuwa aliamua kuanzia chuo hicho kwenye Jengo la Chimwaga lililokuwa mali ya Chama cha Mapinduzi kwa sababu jengo lilikuwa halitumiki ipasavyo. “Unajua tulikuwa tunalitumia jengo hili mara moja ama mara mbili kwa miaka mitano. Kama mkikumbuka hili jengo ndilo lilikuwa limetumike kwa ajili ya Bunge. Ni jengo kubwa sana hili na lilifaa kabisa kuanzia chuo hiki.”Rais Kikwete ametumia zaidi ya saa mbili kutembelea ujenzi wa chuo hicho ambacho kikikamilika kitakuwa na uwezo wa kuchukua wanafunzi kiasi cha 40,000 kwa wakati mmoja.
Akipata maelekezo kuhusu maendeleo ya ujenzi na masomo katika Chuo hicho ambacho tayari kina wanafunzi wapatao 7,000 kutoka kwa Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Kikura, Rais Kikwete ameutaka uongozi wa chuo hicho kubadilisha fikra na kuelekeza nguvu kubwa zaidi katika kukifanya chuo hicho Kituo cha Ubunifu kwa kutoa wasomi wengi zaidi wa shahaha za Uzamili na Uzamivu.
“Kwa kuchukua wanafunzi wachache wa shahada hizo za juu, na wakati mwingine kwa kuongozwa tu na hisia zetu, tunaweza kabisa kuwa tunadumaza maendeleo ya taifa,” amesema Rais Kikwete, akitolewa mfano wa uzoefu wake katika Chuo cha Kenyatta cha Nairobi, ambacho mwishoni mwa mwaka uliopita, kilimtunukia shahada ya heshima za Uzamivu.