Wednesday, January 30, 2013

Polisi Dar wazuia ibada ya Kanisa Moravian Tabata


Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Kipolisi  wa Ilala, Duwani Nyanda akizungumza na viongozi  wa Kanisa la Moravian Jimbo la Misheni Mashariki ambapo polisi walizuia ibada kufanyika jana katika  Kanisa la Moravian Ushirika wa Tabata jijini Dar es Salaam kwa madai kuwa ingehatarisha  amani kwa waumini hao.

POLISI Mkoa wa Kipolisi Ilala, Dar es Salaam jana ulizuia kufanyika kwa ibada kwenye kanisa la Moravian Jimbo la Misheni ya Mashariki Tabata ili kuepusha uvunjifu wa amani.
Kikosi cha polisi kiliongozwa na maofisa wa polisi akiwamo Mkuu wa upelelezi wa kanda hiyo, Duwani Nyanda.
Hatua hiyo ilichukuliwa kutokana na kuwapo kwa mgogoro ambao kwa siku ya jana ungesababisha vurugu kutokana na upande mmoja wa uongozi wa kanisa hilo kutaka kusimikwa kwa nguvu huku upande mwingine ukikataa.
Wakati huohuo Umoja wa Kanisa la Moravian duniani umeukana uongozi mpya uliotangazwa na Mchungaji Clement Fumbo aliyesimamishwa kuwa Mwenyekiti wa Jimbo la Misheni Mashariki kwa madai kuwa umekiuka sheria na katiba za kanisa hilo.
Awali Mchungaji Fumbo alikuwa akipita katika makanisa akitangaza kuwa Umoja wa Kanisa Duniani (Unity Board) unamtambua na kwamba umemruhusu yeye aendelee na uongozi ikiwa ni pamoja na kuchagua halmashauri mpya jambo ambalo ni kinyume na sheria.
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam wakati akitoa maelekezo kwa wachungaji, Mwenyekiti wa Kanisa la Moravian Jimbo la Kusini, Clement Mwaitebele alisema amepokea barua kutoka kwa Mchungaji Dk Jorgen Boytler ikikataa kitendo cha Mchungaji Fumbo kujitwalia madaraka kinyume na katiba.
“Baada ya Mchungaji Fumbo kujichagulia halmashauri yake niliamua kuutaarifu uongozi wa ngazi za juu za kanisa duniani ili kuomba ushauri, ambao nao ulimkana kwa madai kuwa kanisa hilo linaendeshwa kwa kanuni na katiba,” alisema Mchungaji Mwaitebele.
Aliongeza kuwa sehemu ya barua hiyo kutoka kwa Boytler ilisema “Nimepata taarifa kuwa ndugu zetu wa Dar es Salaam wamechagua uongozi mpya wakieleza kuwa ndiyo Halmashauri Kuu mpya ya Jimbo la Misheni Mashariki,  uamuzi huu ni wazi kuwa umekiuka katiba na miongozo yote ya majimbo yetu,” ilisema.
Naye Katibu Mkuu wa Kanisa la Moravian Tanzania, Conrad Nguvumali alikemea vikali hatua hiyo ya Mchungaji Fumbo akisema kuwa ni uasi na usaliti wa hali ya juu na kwamba lazima wachungaji waheshimu uamuzi wa Sinodi.
Source:Mwananchi.co.tz

No comments: