Saturday, November 1, 2008

SEHEMU YA HOTUBA YA RAIS JK KWA WANANCHI JANA:MAOMBI YA WANASAYUNI :LEO TUPO SIKU YA 11

HOTUBA YA JK KWA WANANCHI MWISHO WA MWEZI OKTOBA
HOTUBA YA MWISHO WA MWEZI YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE, KWA WANANCHI TAREHE 31 OKTOBA, 2008

Ndugu Wananchi;Tuanze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia rehema zake tunapata fursa ya kuzungumza mwisho wa mwezi huu Oktoba kwa mujibu wa utaratibu wetu mzuri. Mwisho wa mwezi uliopita sikuweza kuzungumza nanyi kwa sababu ya kuwa New York, Marekani kwa shughuli za kila mwaka za Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.

Suala la OIC

Ndugu Wananchi;
Hivi karibuni kumekuwepo na mjadala usiofurahisha kuhusu suala la Jumuiya ya Kiislamu (OIC) kufuatia taarifa iliyotolewa Bungeni na kwenye vyombo vya habari na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mheshimiwa Bernard Membe.
Nasema isiyofurahisha kwa sababu mjadala huo unaelekea kuchukua sura ya malumbano baina ya waumini wa dini zetu kuu na kupandikiza chuki baina ya serikali na wafuasi wa dini hizo. Ni mjadala unaosikitisha sana jambo ambalo napenda kuwasihi Watanzania wenzangu tusiuendeleze na wala tusiuendekeze.Unaweza kulipeleka taifa letu mahali pabaya.
Napenda kukumbusha kuwa mwaka 1993 Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ilitakiwa kujiondoa kutoka kwenye jumuiya ya OIC baada ya kujiunga kwa hoja kwamba hilo ni shirika la kimataifa ambalo wanachama wake ni mataifa, hivyo kwa hapa nchini kama kungekuwepo na kujiunga iliyostahili kufanya hivyo ni Serikali ya Muungano. Hayo ndiyo matakwa ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hivyo basi Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilijiondoa kwenye OIC na kuiachia Serikali ya Muungano kushughulikia jambo hilo na kuamua ipasavyo.
Tangu wakati huo Zanzibar wamekuwa wanasubiri uamuzi wa Serikali ya Muungano. Kila wakati wenzetu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wamekuwa wanaliuzia suala hilo. Hivi sasa jambo hilo limekuwa mojawapo ya kero kubwa za Muungano zinazoshughulikiwa na Kamati ya pamoja ya Waziri Mkuu na Waziri Kiongozi. Kwa mujibu wa muundo wa Serikali ya Muungano kila kero ya Muungano ina Wizara yake inayohusika nayo kushughulikia. Kwa suala hili ni Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa ndiyo inahusika. Wizara imeamua kufanya utafiti wa jambo lenyewe na wakishakamilisha utafiti huo watoe ushauri kwa Serikali zetu mbili kwa uamuzi.
Ndugu Wananchi;
Nijuavyo mimi, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa haijakamilisha kazi yake ya utafiti na hivyo haijawasilisha Serikalini matokeo ya utafiti wao pamoja na mapendekezo yao kwa ajili ya kutafakariwa na kuamuliwa ipasavyo. Kwa sababu hiyo basi Serikali haijafanya uamuzi wowote kuhusu suala la OIC kwa vile hatujapokea mapendekezo yoyote kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa. Wizara haijamaliza kazi yake. Katika hali hii, nawaomba Watanzania wenzangu tuwe na subira. Tuwaache Wizira ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wafanya kazi yao kwa utulivu ili waishauri Serikali kwa hekima na busara.
Aidha, napenda kuwaomba pia hapo Wizira itakapokamilisha kazi yake (sijui lini) na kuyafikisha mapendekezo yake Serikalini, tuiache Serikali yetu nayo itafakari kwa utulivu ili ifanye uamuzi ya hekima utakaojenga na kulihakikishia taifa letu umoja, amani, utulivu na upendo miongoni mwa raia wa nchi yetu.
Ndugu zangu;
Napenda kuwahakikishia Watanzania wenzangu kuwa siku zote mimi na wenzangu wote Serikalini tunatambua unyeti wa suala la OIC. Aidha, tunatambua dhamana yetu ya kuwa makini katika kufikia uamuzi na kwa uamuzi wenyewe tutakaoufanya kuhusu suala hili. Kamwe hatutafanya uamuzi ambao utavuruga mambo na kuhatarisha amani, umoja na mshikamano wa nchi yetu, Serikali zetu na watu wake.
Hivyo narudia kuwasihi Watanzania wenzangu tuiache Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa ilifanyie kazi kwa ukamilifu suala hili. Tujiepushe na vitendo au kauli ambazo zitawatia watu hofu na kujenga chuki miongoni mwa raia wa nchi yetu wanaopendana na kujenga chuki na kutoaminiana baina ya raia na Serikali yao inayowapenda na kuwathamini.

WAPENDWA WANA SAYUNI.SISI KAZI YETU NI KUOMBA TU.LEO TUPO SIKU YA 11 YA MAOMBI YETU.NENO LA KUSIMAMA NALO NI LILE LILE LA 2NYAKATI 7:14.KAMA UNAPENDA KUUNGANA NA SISI KUHUSU MAOMBI HAYA TUANDIKIE KWENYE EMAIL HII: MIWLC@YAHOO.COM

if my people, who are called by my name, will humble themselves and pray and seek my face and turn from their wicked ways, then will I hear from heaven and will forgive their sin and will heal their land. Now my eyes will be open and my ears attentive to the prayers offered in this place.

No comments: