Tuesday, August 5, 2008

ALIYEKUWA AMEKUFA APATIKANA AKIWA HAI!!

KIJANA aliyejulikana kwa jina moja la Enerico, amepatikana katika pori la Chalinze Wilaya ya Bagamoyo, mkoani Pwani hivi karibuni akiwa amedhoofika mwili kwa kile kinachodaiwa kuwa alikuwa akitumikishwa kazi ngumu na wachawi waliomchukua kimazingara (msukule)
Mwanaume huyo anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 30 hadi 35 alikutwa akiwa na watu wengine ambao walikuwa wakitumikishwa kazi hizo na mwanamke mmoja (jina linahifadhiwa) ambaye alikuwa akiwahifadhi kiuchawi.Zoezi la kupatikana kwa Enerico na wasichana wawili waliojulikana kwa jina moja moja, Jenifa na Sauda ni baada ya mwanamke huyo anayedaiwa kuwa ni mchawi kujisalimisha katika Kanisa la Mchungaji Getrude Rwakatare la Assemblies of God Mikocheni B na kuapa kwamba ameachana na shughuli za kishirikina ili amrudie Mungu.Habari zaidi zinaeleza kuwa kabla ya kupatikana kwa misukule hao, mwanamke huyo alifika kanisani hapo na kutoa ushuhuda mrefu kuhusiana na shughuli zake hizo za kishirikina za kuwachukua vijana wenye nguvu nyingi kwa lengo la kuwafanyisha kazi.Imeelezwa na mmoja wa waliokuwa katika zoezi la kuwarudisha misukule hao ili waishi na jamii kuwa, baada ya mwanamke huyo kutoa ushuhuda wake, jopo la wachungaji wa kanisa hilo walifuatana naye hadi pori la Chalinze na walipofika aliwaita kwa lugha anayotumia akiwahitaji, ambapo walifika na walipoona umati wa watu walitawanyika, wakapotea.Hata hivyo, shuhuda huyo aliendelea kusema kuwa mwanamke yule (mchawi) aliwaita tena na walipofika ndipo wachungaji walifanikiwa kuwakamata Enerico, Sauda na Jenifa huku wakiwa hawana nguo na wakaletwa hadi kanisani hapo kuombewa.Mmoja wa viongozi wa kanisa la Rwakatare ambaye hakupenda jina lake kuandikwa gazetini alisema kuwa, misukule hao waliendelea kuombewa huku wakipata fahamu taratibu na alieleza kuwa Jenifa na Sauda wao walikuwa hawajaathirika sana ubongo kwani akili zao kidogo zilikuwa zikifanya kazi.Taarifa zaidi zinadai vijana hao waliopata fahamu walisema kuwa, wakiwa porini walikuwa wakiishi kwa kula unga wa mtama, nyama na damu za watu iliyokuwa ikipatikana kutokana na ajali ambazo wachawi hao walikuwa wakizisababisha, kitendo kilichofananishwa na cha mtoto Ramadhani mla kichwa ambaye yupo gerezani Segerea kwa tuhuma za mauaji.Habari zaidi zimesema kuwa mwanamke aliyekuwa ‘akiwafuga’ misukule hao alikiri kuwa kuna wakati alikuwa akiishiwa chakula kiasi cha kuwafanya ‘vijana wake’ kuvamia vyakula vya wananchi vijijini bila kuonekana na wanakijiji na raia hao kushangaa kwa nini kilikuwa kinaisha mapema, alibainisha kuwa mlo unapokosekana huwa ni hatari kwani kuna siku walitaka kumpiga.Habari zaidi kutoka kanisani hapo zinasema kuwa, Enerico alitokea Shinyanga vijijini miaka ya nyuma na kuja Bagamoyo kujitafutia maisha.Habari zinasema siku moja alichukuliwa kimazingara huku machoni mwa walio wengi akionekana amekufa na akazikwa huko Bagamoyo baada ya ndugu zake kukosekana.Kwa upande wa Jenifa na Sauda mara baada ya kuombewa na kupata fahamu walieleza walikotoka na tayari ndugu zao wameshapatikana kutoka Bagamoyo. Jamaa zao hao waliwachukua huku wakiwa na furaha ambapo tukio hilo lilioneshwa katika Kituo cha Televisheni cha Channel Ten hivi karibuni.Enerico bado ndugu zake hawajapatikana na umetolewa wito kuwataka wajitokeze kwani hivi sas a fahamu zinaanza kurudia na amekuwa akisali kanisani hapo.Mdau wa kanisa hilo alisema licha ya Enerico, wiki iliyopita mchawi mwingine alimrejesha mwanaume mmoja kanisani hapo ambaye alimchukua kimazingara na kwa sasa ndugu zake wanatafutwa.Mwanamke huyo mchawi hakujitokeza kanisani hapo akihofia usalama wake, lakini inadaiwa kuwa ameamua kuachana na mambo ya kishirikina na kumrudia Mungu.Hivi karibuni vitendo vya ushirikina vimekithiri nchini na kumfanya Rais Jakaya Kikwete kukemea na kuwataka waganga wote wa jadi wawe na vibali vya kufanya shughuli zao na wasijihusishe na mambo ya kishirikina kama vile kukata viungo vya maalbino. Aidha, makanisa nayo yako mstari wa mbele kukemea vitendo hivyo na kuwataka wanaojihusisha navyo kumrudia Mungu.
Source:
globalpublisherstz.com

Haya wapendwa, tuendelee kumwomba Mungu ili aendelee kuwafungua wote waliofungwa na nguvu za giza kila mahali katika nchi yetu-MBARIKIWE!!

No comments: